HABARI MSETO (HEADER)


 


Breaking

March 28, 2026

POLISI YATOA TAHADHARI NA MATAPELI MTANDAONI

Hali ya Usalama nchini inaendelea vizuri kutokana na jitihada za Jeshi la Polisi zinazo saidiwa na ushirikiano mkubwa kutoka kwa wananchi katika kubaini na kuzuia uhalifu.

Pamoja na ushwari huo, yapo matukio mengine yanatendeka kutokana na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii yakiwepo ya utapeli ambayo yameendelea kudhibitiwa.

 

Matukio hayo ya kitapeli ni yale ambayo taarifa zake zimetolewa na baadhi ya wananchi katika Vituo vya Polisi wakilalamika kutapeliwa kupitia mitandao ya kijamii. Taarifa hizo zimeonyesha matapeli wanaofanya uhalifu huo kupitia mitandao ya kijamii wamekuwa wakitumia njia mbalimbali kulaghai watu.

 

Miongoni mwa njia za kilaghai au za kitapeli wanazotumia ni kama vile kutuma jumbe zinazosema "ile fedha tuma kwenye namba hii" ingawaje njia hii na ulaghai huu umeendelea kupungua kwa kiasi kikubwa kutokana na jitihada zinazofanikisha kukamatwa kwa wahalifu waonatumia ulaghai wa aina hiyo na kufutwa au kuondolewa kwa namba za simu walizokuwa wanatumia kwenye mfumo wa mawasiliano.

 

Njia zingine wanazotumia matapeli ni pamoja na kutuma ujumbe wakilaghai ukionyesha umetumwa na kampuni fulani ya simu ukisema; "Huduma zako zote za....zinafungwa leo tarehe....kwa kukosa kurasimisha na kuhakiki namba yako. Kwa msaada piga ofisi zetu za....kwa namba hii  "

Anayetumiwa ujumbe kama huo akipiga namba aliyotumiwa ndipo maneno ya kitapeli yakiwemo ya vitisho kuwa simu yako itafungiwa huanza ikiwepo


kuambiwa afungue viunganishi anavyotumiwa (links) na baadaye huambiwa kuingiza namba yake ya siri/neno siri na akihadaika na kufuata maelekezo anayopewa na kuiingiza neno siri ndipo hujikuta ameibiwa fedha zake. Lakini pia matapeli hutumia njia nyingine ya kumwambia anayetapeliwa atume kiasi cha fedha ili namba yake isifungiwe.

 

Pia, matapeli wengine wamekuwa wakitengeneza akaunti bandia na matangazo kisha kuyasambaza kwenye mitandao wakitumia majina ya Viongozi wa Serikali na Majina ya Wafanyabiashara wakubwa na makampuni yao wakijifanya kuwa, viongozi na wafanyabiashara hao wameanzisha utaratibu wa kukopesha mikopo yenye riba nafuu.

 

Haya yote yanakuwa na malengo ya kutapeli na kuwaibia watakao jiingiza katika mtego huo. Wanaovutiwa na mtego huo huambiwa watume kiasi fulani cha kulipia gharama za kuandaa mkopo huo. Anaye laghaiwa akituma kiasi hicho cha fedha alicho ambiwa, anakijikuta mkopo hapati na anapo jaribu kuwasiliana na aliyekuwa anawasilia naye anakuwa hapatikani tena na simu aliyokuwa anatumia haipo hewani imefungwa.

 

Tahadhari inatolewa kwenu kujihadhari na utapeli wa aina hii na tuendelee kuelimishana kuwa, viongozi wa serikali au wafanyabiashara wakubwa hawawezi kuanzisha makampuni ya kukopesha yasiyokuwa na ofisi maalum zinazojulikana na wala zinazo mtaka mkopaji alipie kiasi fulani cha fedha kwanza ndipo apewe mkopo.

 

Aidha, upo utapeli mwingine unao endelea kupitia mitandao ya kijamii ya matapeli kujifanya kuwa, wanauza bidhaa fulani na hutuma picha kwenye mitandao za bidhaa wanazouza tena kwa bei ambayo ni rahisi kuliko bei za makampuni au wafanyabiashara wanaouza bidhaa kama hizo.

Ulaghai wanaotumia ni kumtaka mhitaji wa bidhaa walizo tuma picha kwenye mitandao awatumie kiasi fulani cha fedha ndipo wawatumie bidhaa husika na akishapokea bidhaa ndipo amalizie kulipa kiasi kilichobakia. Waliofika katika Vituo vya Polisi wameeleza walipotuma kiasi hicho cha fedha walicho ambiwa ndipo walibaini walikuwa wametapeliwa kwani namba aliyokuwa anawasiliana nayo hutoweka na haipatikani tena. Tuchukue tahadhari kubwa sana pale tunapotaka kufanya biashara kupitia mitandao kwa kuhakikisha ni mtu au kampuni halali na sahihi unafanya nayo biashara.

 

Hivyo, Jeshi la Polisi lingependa kuendelea kutoa tahadhari kwa wananchi kujihadhari na utapeli unaofanywa na matapeli wa mtandaoni na kikubwa kuendelea kupeana elimu kuanzia wanaoishi mijini hadi vijijini juu ya utapeli wa aina hizo kwani ndiyo njia pekee na nzuri ya kujikinga na uhalifu na wahalifu wa aina hii.


Jeshi la Polisi litaendelea kutimiza wajibu wake wa kuwasaka na kuwakamata wahalifu wanaojihusisha na uhalifu wa aina yeyote ile na kuwachukulia hatua za kisheria na kwa upande wa wananchi tunatoa wito waendelee kupeana elimu na kuchukuwa tahadhari kabla ya kufanya maamuzi na kamwe tusiongozwe au kusukumwa na tamaa au uharaka wowote ili kujiepusha na mitego ya matapeli mitandaoni.

No comments:

Post a Comment

Pages