Kampuni ya CRDB Insurance Company ikishirikiana na Agriculture and Climate Risk Enterprise (ACRE Africa) imezindua Smart Mifugo, bima inayotumia akili mnemba kuwalinda wafugaji dhidi ya hasara hususan zile zitokanazo na vifo vya ng’ombe.
Akizindua huduma hiyo inayopatikana kupitia
Programu ya DigiBima, jukwaa la
kidijitali linaloratibu usajili, uuzaji na usimamizi wa bima za kilimo na
mifugo kwa wakulima na wafugaji barani Afrika kwa kutumia simu au kishkwambi,
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Agnes Meena amesema Tanzania ni
miongoni mwa nchi chache barani Afrika zenye idadi kubwa ya mifugo, jambo
linaloifanya sekta hii kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi.
Amesema sekta ya mifugo
inatoa ajira na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika upatikanaji wa chakula,
kipato cha kaya, na maendeleo ya viwanda vinavyotegemea mazao ya mifugo ingawa
kuna changamoto zinazoikabili yakiwemo magonjwa, majanga ya asili kama ukame na
mafuriko na hatari nyinginezo zinazosababisha hasara kwa wafugaji wetu.
“Nafurahi kuona ushirikiano
wa CRDB Insurance Company na ACRE Africa umeleta teknolojia ya kisasa kulinda
mali za wafugaji wetu. Kupitia Smart Mifugo, wafugaji sasa wanaweza kupata bima
kwa njia ya kidijitali kwa urahisi zaidi, tena salama na ya uwazi. Matumizi ya
akili mnemba katika kutambua alama ya pua ya mnyama, ni hatua kubwa sana katika
maendeleo ya sekta hii. Ubunifu huu utasaidia kuongeza uaminifu, kupunguza
udanganyifu, na kuboresha utoaji wa huduma za bima,” amesema Agnes.
Serikali inaendelea kuweka
mazingira wezeshi kwa sekta binafsi kuleta ubunifu utakaoongeza tija katika
uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi akisisitiza kuwa Smart Mifugo
inaendana na jitihada za Serikali za kuimarisha maendeleo ya sekta ya mifugo, kuongeza
thamani ya mazao ya mifugo, na kuifanya sekta hii kuwa ya kisasa na yenye
ushindani zaidi.
Akizungumza katika hafla ya
uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela
amesema wameleta ubunifu huo kwa kutambua kwamba sekta ya mifugo ni mhimili
muhimu wa uchumi wa taifa na chanzo cha kipato kwa mamilioni ya Watanzania hivyo
kustahili mazingira salama.
“Wafugaji wetu wanakabiliwa
na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa mfumo madhubuti wa kutambua umiliki wa
mifugo. Hali hii inawanyima fursa ya kupata huduma muhimu kama bima na mikopo.
Kuanzishwa kwa Smart Mifugo ni hatua ya kimkakati ya kukabiliana na
changamoto hizo kwa kutumia teknolojia ya kisasa. Kupitia huduma hiyo, ng’ombe
hutambuliwa kwa kutumia alama ya pua (cow muzzle biometrics), ambayo
hutofautiana kati ya mnyama mmoja na mwingine,” amesema Dkt. Nsekela.
Ubunifu huo, amesema unaondoa utata wa umiliki wa
mifugo, unaongeza uaminifu katika utoaji wa huduma za bima na kuwezesha mifugo
kutambulika rasmi kama mali yenye thamani inayoweza kutumika kama dhamana kupata
mikopo. Dkt. Nsekela amesema baada y auzinduzi huo, huduma hii itapatikana
katika mataifa yote ambako Benki ya CRDB inatoa huduma yaani Burundi na Congo
pia ambako kuna idadi kubwa ya mifugo.
Wakati Smart Mifugo ikiwapa
wafugaji uhakika wa usalama wa mifugo yao dhidi ya hasara na kuwawezesha
kuwatumia ng’ombe wao kama dhamana ya kupata mikopo benki, Dkt. Nsekela amesema
huduma hiyo itachochea ukuaji wa sekta ya mifugo, kuongeza uwekezaji, kupanua
ujumuishaji wa kifedha hususan vijijini, na kuimarisha usalama wa chakula.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB
Insurance Company, Wilson Mnzava amesema ushirikiano wao na ACRE Afrika unaung
amkono dhamira ya Benki ya CRDB kuendeleza ubunifu wa kifedha unaolenga kujenga
uchumi jumuishi na endelevu nchini.
“Tunachoanza leo ni mwanzo tu. Tunaanza na
ng’ombe, lakini tuna matarajio makubwa ya kupanua huduma hii kwa aina nyingine
za mifugo kadri tunavyoendelea,” amesema.
Kwa wafugaji wanaohitaji huduma hii, Mnzava
wanaweza kuipata katika tawi lolote la Benki ya CRDB hivyo akawaomba wadau
kuchangamkia fursa hii ya kuilinda mifugo dhidi ya majanga tofauti kwa uchumi
imara wa familia na jamii nzima ya wafugaji kwa ujumla.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa
ACRE Africa, Ewan Wheeler amesema Tanzania ina takriban ng’ombe milioni 40
wenye thamani ya dola za Marekani bilioni 4.5 ila sehemu kubwa ya utajiri huu
upo kwenye sekta isiyo rasmi hivyo kuhitaji mikakati ya pamoja na kuirasmisha.
“Wafugaji wanahangaika sana
kupata bima na mikopo kwa dhamana ya mifugo yao kutokana na ugumu wa kuitambua
lakini kwa kutumia akili mnemba jambo hilo limepata suluhisho sasa hivi. Kwa
kurahisisha utambuzi wa mifugo, taasisi za fedha zitakuwa na Imani kubwa ya
kurudisha fedha zao hivyo kuwakopesha wafugaji watakaokuza ufugaji na kuongeza
tija ya sekta ya mifugo nchini,” amesema Wheeler.




No comments:
Post a Comment