Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo
amefungua rasmi Jukwaa la Biashara Tanzania-Urusi jijini St. Petersburg na kutoa wito
kwa wawekezaji, viongozi wa biashara na taasisi kutoka nchi hizo mbili kutafsiri urafiki
wa muda mrefu kuwa ushirikiano halisi wa kiuchumi na uwekezaji.
Akilihutubia Jukwaa hilo lililofanyika pembezoni mwa Jukwaa la 29 la Kimataifa la
Uchumi la St. Petersburg (SPIEF 2026), Rais Samia alisisitiza kuwa Tanzania na Urusi
zimekuwa na uhusiano imara wa kidiplomasia kwa zaidi ya miongo sita, lakini
akabainisha kuwa ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara bado haujafikia uwezo wake
kamili.
“Kiwango cha sasa cha biashara kati ya Tanzania na Urusi hakiendani na hadhi ya
uhusiano wetu wa pande mbili. Hapa si mahali tunapopaswa kuwa,” alisema Rais Samia.
Rais Samia amesema kuwa licha ya nchi hizo mbili kujenga msingi imara wa kuaminiana
na kushirikiana kwa miaka mingi, sasa umefika wakati wa kuelekeza nguvu katika
matokeo ya vitendo, kuongeza uwekezaji na kupanua biashara.
Dkt Samia alieleza kuwa Jukwaa hilo ni fursa muhimu kwa jumuiya za biashara za
Tanzania na Urusi kuzungumza moja kwa moja, kutambua fursa zilizopo na kujenga
ushirikiano utakaotoa manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Akizungumza awali katika Jukwaa hilo, Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho
la Urusi, Mheshimiwa Maxim Reshetnikov, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa
washirika wenye fursa kubwa zaidi kwa biashara za Urusi barani Afrika kutokana na
ukuaji wake imara wa uchumi, utajiri wa rasilimali asilia, idadi kubwa ya vijana na nafasi
yake ya kimkakati kama lango la masoko ya kikanda.
Alibainisha kuwa biashara kati ya nchi hizo mbili ilifikia kiwango cha juu zaidi kuwahi
kufikiwa mwaka 2025 na kueleza utayari wa Urusi kuongeza uagizaji wa kahawa,
tumbaku, parachichi, karanga na matunda kutoka Tanzania, huku ikipanua mauzo ya
mbolea, ngano, mafuta ya alizeti na pembejeo nyingine za kilimo.
“Tanzania ni mshirika mwenye matumaini makubwa kwa kampuni za Urusi. Ni miongoni
mwa nchi za Afrika zenye ukuaji thabiti wa uchumi, rasilimali nyingi na idadi kubwa ya
vijana,” amesema Waziri Reshetnikov.
Mheshimiwa Reshetnikov pia alitangaza kuwa Urusi iko tayari kwenda zaidi ya biashara
ya kawaida na kuingia katika uzalishaji wa pamoja na uwekezaji, hususan katika sekta za
kilimo, madini, nishati, afya, miundombinu ya usafiri na teknolojia za kidijitali.
Akizungumzia nguvu ya uchumi wa Tanzania, Rais Samia alisema nchi inaendelea kuwa
na ukuaji mzuri wa uchumi, utulivu wa uchumi jumla na nafasi ya kimkakati
inayowezesha kufikia soko la zaidi ya watu milioni 500 katika Afrika Mashariki na Kusini.
Dkt. Samia alieleza kuwa uwekezaji unaoendelea katika bandari, reli, shoroba za
usafirishaji na miundombinu ya viwanda ni miongoni mwa nyenzo muhimu
zinazowezesha biashara na uwekezaji.
Rais Samia alitaja sekta za madini, kilimo, mafuta na gesi, nishati, afya, dawa, usafirishaji
na usafirishaji wa mizigo kuwa miongoni mwa maeneo yenye fursa za haraka kwa
ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi.
Katika sekta ya madini, aliwaalika wawekezaji wa Urusi kushiriki katika tafiti za kijiolojia,
uchakataji wa madini, ujenzi wa mitambo ya kuyeyusha na kusafisha madini, huku katika
sekta ya kilimo akihamasisha uwekezaji katika uzalishaji wa mbolea, teknolojia za kilimo
na kuongeza thamani ya mazao.
Rais Samia pia alieleza fursa zilizopo katika maendeleo ya gesi asilia, utengenezaji wa
bidhaa za dawa, maendeleo ya miundombinu na ushirikiano katika teknolojia za nishati.
Mheshimiwa Rais pia alitumia Jukwaa hilo kutangaza kuanza rasmi kwa safari za ndege.
“Ninafurahi kutangaza kwamba Air Tanzania itaanza safari za moja kwa moja kati ya
Dar es Salaam, Moscow na Zanzibar tarehe 2 Julai 2026. Hii ni hatua muhimu katika
kuimarisha biashara na utalii kati ya nchi zetu.”
Akitoa wito wa kuongeza kasi ya utekelezaji, Dkt. Samia alisema: “Kuzungumza pekee
hakutazaa matunda. Tunapaswa kubadili majadiliano yetu kuwa vitendo.”
Aidha, alisisitiza dhamira ya Serikali yake ya kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji
na kuimarisha zaidi mahusiano ya kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.
Jukwaa hilo limewakutanisha viongozi waandamizi wa serikali, wawekezaji, viongozi wa
biashara na wawakilishi wa sekta binafsi kutoka Tanzania na Urusi.
Jukwaa hili linafuatia mafanikio ya Jukwaa la Biashara Urusi–Tanzania lililofanyika jijini
Arusha mwezi Aprili 2026, ambalo liliwakutanisha zaidi ya kampuni 150 za Urusi na
wafanyabiashara wa Tanzania kujadili fursa za uwekezaji katika sekta za kilimo, madini,
nishati, utalii, miundombinu, TEHAMA na viwanda.
Miongoni mwa maeneo muhimu yaliyotambuliwa kwa ushirikiano ni uzalishaji na
uchakataji wa mazao ya kilimo, utengenezaji wa mbolea, uchimbaji na uongezaji thamani
wa madini, maendeleo ya gesi asilia, dawa na vifaa tiba, teknolojia za kidijitali, usalama
wa mtandao, utalii, miundombinu ya usafirishaji na elimu.





No comments:
Post a Comment