HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 24, 2015

JK APOKEA MSAADA WA VITABU VYA SAYANSI NA HISABATI

Rais Jakaya Jakaya Kikwete akipokea sehemu ya msaada wa vitabu milioni 2.5 vya hisabati na sayansi kutoka kwa balozi wa Marekani, Mark Childress wakati hafla iliyofanyika katika Shule ya Sekondari Mtakuja iliyopo Kunduchi  jijini  Dar es Salaam. (Picha na Francis Dande)

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mtakuja wakiimba ngojera wakati wa hafla ya makabidhiano ya vitabu milioni 2.5 vya Hisabati na Sayansi vilivyotolewa na Serikali ya Marekani kwa ajili ya shule ya sekondari za Tanzania.

Na Mwandishi Wetu

RAIS Jakaya Kikwete  amesema shule za Sekondari 3,551 za Serikali nchini  zimegawiwa vitabu vya masomo ya Sayansi milioni 2.5 kutoka nchi ya Marekani ili kupunguza uhaba wa vitabu mashuleni.
Makabidhiano hayo yalifanyika jana katika shule ya Sekondari Mtakuja iliyopo Kunduchi Dar es Salaam, waliowakilisha shule zote za sekondari nchini na kusababisha kuongeza idadi ya vitabu kwa uwiano wa wanafunzi wawili kitabu kimoja na katika shule nyingine mwanafunzi mmoja kwa kitabu kimoja.
Kikwete alisema  huo ni muendelezo wa Sera ya elimu iliyozinduliwa hivi karibuni  katika shule ya msingi Majani ya chai iliyopo Ilala jijini Dar es Salaam, na kuahidi kuwa tatizo la vitabu mashuleni kwa sasa ni historia.
Alisema changamoto kubwa iliyopo kwa sasa ni ukosefu wa walimu wa sayansi kwa idadi ndogo ambapo kwa mwaka 2005 kulikuwa na walimu 500 lakini hadi kufikia mwaka 2014 kuna idadi ya walimu 18,000 wa masomo ya sayansi na wengine 18,000 wakisubiri ajira zao.
Alisema upungufu wa walimu wa sayansi kwa sasa unatokana na vyuo vingi kukosa nafasi ya kuchukua walimu wengi wa masomo hayo kwa mkupuo  lakini jitihada za Serikali zinafanyika katika kuhakikisha kuwa walimu wanapata nafasi mbalimbali za masomo hasa katika mataifa ya nje.
Rais Kikwete pia aliendelea na kuwapa walimu ahadi kem kem ikiwa ni pamoja na kuwajengea nyumba zao mijini na vijijini ,kuongeza ajira katika masomo ya Sayansi huku akiwataka walimu kujiendeleza katika masomo hayo kwa kuwa huko mbele ajira zitakuwa za kumwaga.
Akizungumzia shule ya Sekondari ya Mtakuja ambayo ndio ilikabidhiwa vitabu hivyo kwa niaba ya shule nyingine nchini alisema kuna uhaba wa walimu nane wa sayansi ambapo alimuagiza Naibu wa  Waziri wa Tamisemi anayeshughulikia elimu Kassim Majaliwa kuhakikisha shule hiyo inapatiwa walimu wa sayansi.
Hata hivyo aliwataka walimu kutovunjika moyo huku akiwaambia kwamba endapo atamaliza muda wake wa urais hata Mkewe mama Salma Kikwete ambaye aliambatana naye atarudi shuleni kufundisha hatua iliyopelekea walimu kushangilia kwa shangwe.
Naye Balozi wa Marekani Nchini Tanzania Mark Childress alisema kuna umuhimu mkubwa wa kuimarisha stadi za msingi kwa wanafunzi ambao ni pamoja na kusoma ,kuandika na kuhesabu ili kuwawezesha kuelewa vyema maudhui ya vitabu hivyo na kuweza kuvitumia kikamilifu.
Alisema Serikali ya Tanzania na Marekani zinachukua jitihada za pamoja katika kuweka msingi imara wa stadi mbalimbali kwa kutoa elimu bora,sio tu katika masomo ya sayansi bali katika kuandika ,kusoma na kuhesabu.
Balozi huyo alisema lengo la Serikali ya Marekani ni kusaidia Tanzania program mbalimbali zinazolenga kuongeza fursa za elimu kwa wasichana kumethibitisha kuleta mafanikio makubwa na endelevu ya kiuchumi.
Naye Meya wa Manispaa ya Kinondoni Yusuf Mwenda alisema kuwa awali manispaa hiyo ilikuwa na shule tano tu lakini hadi sasa kuna shule 49 ambazo ni sawa sawa na ongezeko la shule 44 sawa na asilimia 840.
Kukabidhiwa kwa vitabu hivyo kunafuatia mradi mwingine kama huo uliofadhiliwa na USAID  hapo mwaka 2008,ambapo kwa kupitia ushirikiano kati ya chuo Kikuu cha South Calorina na Wizara ya Elimu ya Zanzibar  ambapo zaidi ya vitabu milioni moja na zana nyingine za kujifunzia ziliandaliwa na kusambazwa visiwani humo.

No comments:

Post a Comment

Pages