HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 22, 2015

Msama amwangukia JK mauaji ya albino


MKURUGENZI wa Kampuni ya Msama Promotions ya jijini Dar es Salaam, Alex Msama akikabidhi misaada kwa mmoja wa viongozi wa vituo vitano vya kulea yatima ikiwa ni utaratibu wa kusaidia makundi maalumu. Msaada huo uliotolewa jana katika Ofisi za Gazeti la Dira Mtanzania, Kinondoni, ni sehemu ya mapato ya Tamasha la Pasaka la mwaka 2014. (Picha na Loveness Bernard)

NA MWANDISHI WETU

MWENYEKITI wa Kampuni ya Msama Promotions ya jijini Dar es Salaam, Alex Msama, ameelezea kuguswa kwake na wimbi la mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi akisema kuwa ni ukatili uliopitiliza, ambao hata wanyama wa jamii moja hawawezi kufanyiana huku akitoa wito kwa serikali kuongeza kasi ya kupambana na laana hiyo inayolinyemelea taifa. 

Msama alisema haiingii akilini kuona watu wakifanya ukatili wa kiwango cha kutisha eti kwa imani kuwa wakifanya hivyo wanaweza kupata mafanikio ya utajiri katika maisha yao bila kutambua kuwa huko ni kutafuta laana ya Mungu kwa sababu vitendo hivyo si tu havipendezi mbele ya Mungu, bali hata machoni pa wanadamu.

Msama ambaye ni miongoni mwa wadau wa kuhimiza amani na upendo katika jamii ikiwa ni moja ya malengo ya matamasha ya Injili ambayo amekuwa akiyaratibu tangu mwaka 2000, aliyasema hayo jana wakati akitoa misaada ya kiutu kwa vituo vitano vya kulea yatima vya jijini Dar es Salaam kuelekea Tamasha la Pasaka la mwaka huu.

Katika hafla hiyo iliyofanyika ofisini kwake eneo la Kinondoni na kuhudhuriwa na watoto na viongozi wa vituo hivyo pamoja na wadau mbalimbali wa masuala ya kijamii, Msama alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa jamii kuyasaidia makundi maalumu kama watoto yatima na walemavu kwa ujumla wake wakiwamo albino waliopo katika hatari kubwa.

Msama ametoa wito kwa serikali kuongeza kazi na mbinu mpya za kupambana na watu wanaojihusisha na vitendo hivyo ambavyo si tu ni ukatili uliopitiliza na ukiukwaji wa haki za binadamu na mafundisho ya Neno la Mungu, pia ni vitendo vinavyolipaka matope taifa katika uso wa kimataifa.

Alikwenda mbali na kushauri serikali kuona umuhimu wa kubuni njia bora ya kuwanusuru watoto wenye ulemavu huo kwa namna yoyote, ikiwezekana kijengwe kituo maalumu cha kuwatunza, pia hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi ya wahusika wa mauaji hayo ambayo yanakwenda kinyume cha haki ya mtu kuishi na kuthaminiwa utu wake. 

Msama amesema kwa usikivu wa Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais  Jakaya Kikwete, anamsihi kabla ya kumaliza kipindi chake baadaye mwaka huu angeliangalia upya suala hilo kwa lengo la kuepusha uhai wa jamii hiyo inayoishi kwa hofu kubwa juu ya usalama wao.  

“Najua Rais wetu mpendwa (Jakaya Kikwete) ni msikivu na mwenye huruma na makundi haya maalumu katika jamii,
sisi waratibu wa Tamasha la Pasaka tungemsihi suala hili la mauaji ya albino litafutiwe dawa huku watoto wenye ulemavu wa ngozi (albino) wakijengewa makazi yao maalumu,” alisema.

Alisema kwa vile suala la amani na upendo ni moja ya ajenda ambazo zimekuwa zikihimizwa kupitia Tamasha la Pasaka, wataendelea kuhimiza vita dhidi ya vitendo hivyo vibaya si tu mbele za Mungu, bali hata machoni mwa wanadamu, ili Tanzania iendelee kuwa sehemu salama ya kuishi.

Mapema mwezi huu, mwili wa mtoto albino, Yohana Bahati (mwaka mmoja) aliyekuwa ameporwa kutoka mikononi mwa mama yake katika Kijiji cha Lumasa, Wilaya ya Geita, Mkoa wa Geita, ulipatikana katika pori la Hifadhi ya Biharamulo, lililoko Wilaya ya Biharamulo, Mkoa wa Kagera, ukiwa umenyofolewa mikono na miguu.

Kuhusu misada, Msama jana alikabidhi misaada ya vitu mbalimbali vikiwamo unga, mafuta ya kupikia, mafuta ya kupaka, sabuni na sukari kwa vikundi hivyo vitano, misaada yote ikiwa na thamani ya shilingi mil. 5; ikiwa ni kutambua wajibu wa jamii nzima katika kuyasaidia makundi maalumu.

Vituo vilivyopata msaada huo ni  Malaika Kids, Honoratha, Maunga Centre, Mwandaliwa na Istikama, vyote vya jijini Dar es Salaam, ambapo baada ya kukabidhi, Msama alitoa wito kwa wengine wenye uwezo na jamii kwa ujumla kujenga utamaduni wa kusaidia wenye mahitaji maalumu.

Msama Promotions wametoa msaada huo wakiwa katika maandalizi ya Tamasha la Pasaka litakaloanzia jijini Dar es Salaam, Aprili 5 kabla ya kusambaa katika mikoa mbalimbali likibeba malengo mbalimbali, ikiwemo shangwe za miaka
15 tangu lianzishwe.

No comments:

Post a Comment

Pages