Waziri Mkuu,
 Kassim Majaliwa akijadili jambo na Afisa Mtendaji  Mkuu wa Kampuni  ya 
Simu Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba kabla ya kuanza mkutano kwa njia 
 ya video na  Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa na Waganga Wakuu 
wa Mikoa  akiwa ofisini kwake, Mlimwa jijini Dodoma, Machi  21, 2020. 
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Wakuu 
wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa  na Waganga Wakuu wa Mikoa kwa njia 
ya video akiwa ofisini kwake Mlimwa jijini Dodoma, Machi 21, 2020. 
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
Na Mwandishi Wetu
WAZIRI
 MKUU Kassim Majaliwa ameonya juu ya upotoshwaji na utoaji holela wa 
taarifa kuhusu ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababisha na virusi vya 
corona (COVID 19) unaofanywa na watu mbalimbali nchini.
Amesema
 kuanzia sasa taarifa hizo zitatolewa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya 
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na ikilazimika zitatolewa na Waziri Mkuu 
na ikilazimika sana zitatolewa na viongozi wakuu wa nchi ili kuepusha 
mikanganyiko.
Waziri
 Mkuu ametoa onyo hilo leo (Jumamosi, Machi 21, 2020) wakati akizungumza
 na Wakuu wa Mikoa yote nchini, Makatibu Tawala wa Mikoa na Waganga 
Wakuu wa Mikoa kwa njia video kutokea ofisini kwake Mlimwa, jijini 
Dodoma.
Kufuatia
 hali hiyo, Waziri Mkuu ameiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
 ifuatile watu wote wanaofanya upotoshaji kwa kupitia mitandao ya 
kijamii ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.
“Watu
 wote wanaopotosha umma na kuleta taharuki kuhusu ugonjwa wa corona 
badala ya kuelimisha namna ya kujikinga, wafuatiliwe na kuchukuliwa 
hatua,” amesisitiza.
Waziri
 Mkuu amesema licha ya hali ya maambukizi ya corona nchini kutia 
matumaini, viongozi hao hawana budi kupeana taratibu za namna ya 
kukabiliana na tatizo hilo. 
“Wakuu
 wa mikoa kila mmoja ahakikishe eneo lake linakuwa salama na endapo 
kutakuwa na mgonjwa tumieni zahanati ambazo bado hazijaanza kutumika kwa
 ajili ya kutolea huduma kwa wagonjwa wa corona,” amesema.
Amewataka
 wakuu hao wa mikoa waimarishe utoaji wa elimu kwa umma na ikiwezekana 
watumie magari ya matangazo ili wananchi waelewe athari za ugonjwa huo 
na namna ya kujikinga pamoja na kuwaondolea hofu ili waweze kuendelea na
 shughuli zao za kimaendeleo. 
Pia
 amewataka watumie redio za kijamii katika maeneo yao kutoa elimu kwa 
umma juu ya kujikinga na ugonjwa huo na wasimamie maeneo ya utoaji 
huduma kama vituo vya mabasi na kuhakikisha kila abiria anakaa kwenye 
kiti. 
“Nendeni
 kwenye maeneo ya mikusanyiko, vituo vya mabasi kutoa elimu kwa umma na 
kuwaondoa hofu. Upande wa maofisini, viwandani na kwenye mgodi kuwe na 
utaratibu wa kutoa elimu kwa wafanyakazi kila siku asubuhi watumie hata 
robo saa kabla ya kuanza kazi waelekezwe namna ya kujikinga.”
Waziri
 Mkuu amesema kwa wanaoishi katika maeneo ya makambi, viongozi wao 
waelekezwe namna ya kutoa elimu ya kujikinga na corona na pia wadhibiti 
utorokaji na Serikali kwa upande wake inaendelea kuimarisha udhibiti 
mipakani, uwezo wa kupima sampuli na upatikanaji wa vifaa.
Amewataka wakuu hao wa mikoa, wawashirikishe wakuu wa wilaya kwenye mikoa yao ili wasimamie utekelezaji wa maagizo hayo.
Wakati huohuo,Waziri
 Mkuu amewaagiza wakuu hao wa mikoa wahakikishe wanawafuatilia na 
kuwachukulia hatua wafanyabiashara wote watakaobainika kuongeza bei kwa 
bidhaa ambazo zinatumika katika udhibiti wa maambukizi ya ugonjwa wa 
corona.
Kuhusu
 viongozi wa dini, Waziri Mkuu amewaomba waendelee kushirikiana na 
Serikali katika kuwaelimisha waumini wao wote kuzingatia tahadhari za 
ugonjwa huu. Pia awaendelee kuliombea Taifa. 
 
 
 
 

 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment