Katibu
Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba amesema kuwa Tume ya
Madini imeendelea kubuni mikakati mbalimbali ya kuhakikisha inavuka
lengo ililopewa la kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 650 kwa mwaka wa
fedha 2021-2022 ifikapo Juni mwaka huu ikiwa ni pamoja na kuimarisha
usimamizi kwenye shughuli za uchimbaji na biashara ya madini na kuongeza
vitendea kazi.
Mhandisi
Samamba aliyasema hayo leo kwenye ziara ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara
ya Madini, Msafiri Mbibo kwenye Ofisi za Tume ya Madini Makao Makuu
jijini Dodoma ambapo alikutana na viongozi wa Tume kwa lengo la
kujifunza majukumu ya Tume na kutatua changamoto mbalimbali.
Alisema
kuwa katika kuimarisha Sekta ya Madini nchini hadi kufikia tarehe 23
Februari, 2022 jumla.ya magari saba yalipokelewa na kuongeza kuwa magari
mengine 33 yapo njiani ikiwa ni kama mkakati wa kuhakikisha Tume
inapata vitendea kazi vya kutosha katika kusimamia Sekta ya Madini.
Alieleza
mikakati mingine kuwa ni pamoja na kusogeza huduma karibu na wananchi
ikiwa ni pamoja na uanzishwaji wa Ofisi za Maafisa Madini Wakazi wa
Mikoa 29, Ofisi za Maafisa Migodi Wakazi 13 pamoja na Maabara moja ya
kufanya tathmini ya sampuli za madini, kuchambua na kuthaminisha madini
yanayozalishwa iliyopo jijini Dar es salaam.
Aliongeza
mikakati mingine kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa masoko 42 na vituo
vidogo vya ununuzi wa madini 70 nchini, kati ya masoko hayo 27 ni ya
madini ya dhahabu, masoko 14 ya madini ya vito na soko moja la madini
ya bati.
Katika hatua
nyingine akielezea hali ya ukusanyaji wa maduhuli kwa Mwaka wa Fedha
2021-2022, Mhandisi Samamba alisema kuwa kuanzia kipindi cha mwezi Julai
2021 hadi Februari, 2022 Tume imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi
bilioni 412.27 sawa na asilimia 63.4 ya lengo la mwaka husika.
Alisema
pia mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa mwaka 2020 ulikua
hadi kufikia asilimia 6.7 kutoka asilimia 4.8 mwaka 2018.
Katika
hatua nyingine, Mhandisi Samamba aliishukuru Wizara ya Madini kupitia
viongozi wake kwa msaada mkubwa hususan kwenye utatuzi wa changamoto
mbalimbali zinazoikabili Tume.
Naye
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula alisisitiza kuwa
Tume ya Madini imejipanga kuhakikisha inafikia lengo la ukusanyaji wa
maduhuli lililowekwa na kuwataka watumishi wa Tume kuendelea kuchapa
kazi kwa ubunifu na uadilifu mkubwa.
Profesa
Kikula sambamba na kupongeza uteuzi wa Naibu Katibu Mkuu aliahidi
ushirikiano wa Tume katika kuhakikisha Sekta ya Madini inazidi kuwa na
mchango mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi kupitia ukusanyaji wa
maduhuli, usimamizi wa karibu kwenye shughuli za uchimbaji na biashara
ya madini na kuhakikisha watanzania wananufaika na uwekezaji kwenye
shughuli za madini nchini.
Wakizungumza
kwa nyakati tofauti Makamishna wa Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim
Mruma na Janeth Reuben Lekashingo walisema Tume ipo tayari kushirikiana
na Wizara ya Madini kwenye maboresho ya sheria na kanuni lengo likiwa ni
kuhakikisha watanzania wanaendelea kunufaika kwenye Sekta ya Madini.
Kamishna
wa Tume ya Madini, Janeth Lekashingo aliongeza kuwa katika kuhakikisha
watanzania wanakuwa na uelewa mpana wa fursa zilizopo kwenye Sekta ya
Madini, Tume imekuwa ikitoa elimu mikoa mbalimbali kuhusu ushirikishwaji
wa watanzania kwenye Sekta ya Madini na kusisitiza zaidi kuwa elimu
itaendelea kutolewa katika mikoa mingine yote.
Wakati
huohuo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo amewataka
watumishi wa Tume ya Madini kuendelea kuchapa kazi kwa ubunifu na
uadilifu mkubwa ili mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa
uendelee kukua kwa haraka.
"Bado
ninaamini Tume ya Madini inaweza kufanya vizuri zaidi ya hapa,
endeleeni kuchapa kazi kwa ubunifu na uadilifu huku mkiwa wazalendo
katika mazingira ya aina yoyote kama wanajeshi," alisema Mbibo.
Katika
hatua nyingine Mbibo alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini
itaendelea kutatua changamoto zilizopo kwenye utendaji wa Tume ya
Madini lengo likiwa ni kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi na
kuvutia wawekezaji zaidi nchini.
No comments:
Post a Comment