HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 13, 2022

Serikali yatenga Bilioni Moja kuchochea Sekta ya Vitabu

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB.
Baadhi ya wadau wa elimu nchini wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Tanzania Dkt. Aneth Komba akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo.

 
Na Hussein Ndubikile, Dar es Salaam

Serikali imesema kuwa imetenga Shilingi bilioni moja kwa Mwaka wa Fedha 2022/23 ili kuchochea ukuaji wa Sekta ya Vitabu nchini ikiwemo usomaji, uchapishaji na kufufua soko la vitabu ambayo hali yake si ya kuridhisha. 


Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda katika Hafla ya Uzinduzi wa Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu ambayo mshindi atatangazwa Aprili 13, 2023 siku ambayo ni Kumbukumbu ya kuzaliwa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.


Waziri Mkenda amebainisha kuwa hali ya uchapaji na usambazaji wa vitabu vya ziada vyenye ithibati nchini si ya kuridhisha hivyo Serikali imeamua kwamba itasimamia uchapishaji, kuvinunua na kuvisambaza mashuleni hadi Maktaba ya Taifa vitabu vya mshindi wa tuzo hiyo.


Profesa Mkenda amesema kuwa kupitia tuzo hiyo Serikali inafungua ukurasa wa kuchochea hari mpya katika uchapishaji na usomaji wa vitabu nchini pamoja na kuchangamsha soko la vitabu nchini.


“Tumetenga kwenye bajeti kiasi cha Sh bilioni moja kwa ajili ya kuhakikisha tunaanzia kutekeleza mapendekezo ya wadau wetu na taratibu zote zitafanyika chini ya Taasisi ya Elimu Tanzania(TET) lengo ni kukidhi matakwa ya wadau kuchangamsha soko siyo kushuhudia baadhi ya taasisi za uchapashaji zinafungwa,” amesema Prof. Mkenda na kuongeza kuwa,


“Lakini pia ili watu wasome lazima wajue vilivyomo ndani na tunataka tutumie utaratibu huu kukuza Kiswahili ndiyo maana uandishi utatumia Kiswahili tutaanza na uandishi wa Riwaya na Mashairi baadaye tutakuja na Tamthilia na Hadithi fupi fupi,”.


Kwa upande wake Kamishna Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Lyabwene Mtahabwa kwa niaba ya Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Francis Michael amewasisitiza Waandishi wa vitabu kuandika kuhusu watoto kwani wamekuwa wakipitia changamoto ya mazingira magumu kwa kufanyiwa vitendo viovu ndani ya Jamii na wahusika ni ndugu zao wa karibu vitendo hivyo ni pamoja na kulawitiwa kubakwa, kupigwa, kunyanyapaliwa hivyo wakiandika vitabu itasaidia kubadilisha Jamii.


“Watoto ni tunu kubwa tuliyopewa na Mwenyezi Mungu kuwa baraka lakini leo tukiwaangalia baadhi ya watoto wanavyoteseka kutokana na changamoto wanazokutana nazo machozi yananitoka kila nikisoma magazeti visa na mikasa yao ni vya kutisha kalamu yenu itawaokoa”. amesema Prof. Mtahabwa.


Nae, Mwenyekiti Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Profesa Penina Mlama amesema Mbunifu atakayeshiriki atatakiwa kuandika nyanja moja tu kwa mada atakayoichagua yaani riwaya au ushairi na andiko liwe makini litakalojikita katika masuala ya kijamii na dirisha ya kuwasilisha kutakuwa wazi kuanzia Septemba 13- Novemba 30 mwaka huu.


Aidha amesema majaji watapitia maandiko ya kila mshiriki atakayetuma kupitia barua pepe na zawadi nono Kwa washindi itakuwepo ambapo mshindi wa kwanza atapewa kiasi cha Sh milioni 10 huku wa pili akipatiwa Sh milioni 7 na watatu atapewa Sh milioni 5 hivyo waandishi wote wa vitabu waandike kazi nzuri na hii kwani tuzo hizo zitakuwa kila mwaka .


Mkurugenzi Mkuu wa TET Dkt. Aneth Komba amempongeza Prof. Makenda kwa ubunifu wake wa kuanzisha tuzo hiyo yenye lengo la kukuza Sekta ya Uandishi na kuongeza ari ya kujisomea.


Ameahidi kuwa watahakikisha wanasimamia tuzo hiyo kwa ili kufikia malengo makubwa yaliyokusudiwa.

No comments:

Post a Comment

Pages