WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yussuf Masauni amesema miongoni mwa mafanikio makubwa yaliyopatikana ni kutatuliwa kwa hoja za Muungano chini ya Ofisi hiyo.
Amesema
hayo wakati akifafanua hoja mbalimbali za wabunge waliochangia hotuba ya bajeti
kwa mwaka wa fedha 2026/27 aliyoiwasilisha bungeni jijini Dodoma Aprili 21,
2026.
Mhandisi Masauni alisema kuwa katika kipindi cha miaka
mitano ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia hoja 11 zimetatuliwa hadi kubakia
hoja tatu ambazo hivi karibuni mbili kati yake zinatarajiwa kutatuliwa kupitia
vikao vya Kamati ya pamoja ya Serikali zote mbili.
“Mheshimiwa Mwenyekiti na ndugu zangu Waheshimiwa
Wabunge tunakwenda kuifanya Ofisi ya Makamu wa Rais kuwa ya kuzungumzia fursa
na si hoja za Muungano,” alisisitiza.
Aidha, Mhandisi Masauni alisema kuwa Ofisi imekuja na
mpango kabambe wa elimu kwa umma kuhusu Muungano ambao unalenga mambo mengi huku
mojawapo linagusia mambo ya vijana.
Aliongeza kuwa amezingatia maoni ya wabunge kuhusu
utoaji wa elimu ya Muungano ambapo alibainisha kupitia midahalo, mitandao ya
kijamii elimu inatolewa na ndio maana zimetengwa fedha kwa ajili ya kuanzisha
makavazi jijini Dodoma na Dar es Salaam ili kuhifadhi kumbukumbu za Muungano.
Katika kulipa nguvu ya kuwa mamlaka kamili Baraza la
Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Waziri Masauni alifafanua
kuwa suala hilo lipo kwenye hatua nzuri na ni matarajio kuwa Bunge lijalo
sheria itapelekwa bungeni kwa ajili ya kupitishwa.
“Si kuifanya NEMC kuwa mamlaka kamili bali tunataka kuifanya
NEMC kuwa ya kisasa zaidi, kupata vitendea kazi kama vile magari ya kutosha,
mifumo ya kisasa kung’amua wapi kuna changamoto za kimazingira, tuwe na drones, boti za kisasa za kufika maeneo
yote na tunataka katika kanda zote tuwe na vituo vya umahiri kama ilivyo kanda
ya Geita,” alisema.
Kuhusu Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC),
alisema ni kweli bado fursa za biashara ya kaboni hazijatumika ipasavyo hivyo
mkakati uliopo ni kuifanya biashara hiyo kuwa ni chanzo mojawapo cha mapato kwa
kuingiza shilingi bilioni mbili kwa mwaka.
Awali akichangia hotuba hiyo, Naibu Waziri Ofisi ya
Makamu wa Rais Mhe. Reuben Kwagilwa alisema kuwa Nguzo ya kwanza ya Dira 2025 inazungumzia
uchumi imara jumuishi na shindani ambayo inazingatia uchumi unaokua kwa kasi
unaobebwa na sekta binafsi.
Aidha, alieleza nguzo ya pili ni uwezo wa watu na
maendeleo ya jamii ya kitanzania
inayoweza kuwa na afya, elimu bora na ujuzi kwa ajili ya kuendna na soko
la ajira la dunia ya sasa.
Hivyo, alisema ili kuhakikisha yote haya yanafanyika
nguzo ya tatu ni uendelevu wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya
tabianchi ambayo imewekwa ili kusimamia rasilimali za taifa.
“Tumekaa na wataalamu tumekubalina tutumie dhamana hii
ya kusimamia mazingira na taifa kwa ajili ya vizazi tunakwenda kuifanya kwa
ufanisi, Mheshimiwa Rais ambaye ni kinara kwa mazingira Tanzani, Afrika na dunia
amesaini kitabu hiki cha Dira anataka nguzo hizi zituelekeze kwenye uchumi wa
dola trilioni moja kuhudumia watanzani ambao mwaka 2050 tutakuwa milioni 118 na
pia anatakja tuwe na uchumi wa juu wa pato la kati.,” alisema Mhe. Kwagilwa.
Kwa hatua hiyo, Bunge la Jamhuri la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, limepitisha bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais yenye jumla
ya shilingi bilioni 99.9 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli zake katika mwaka
wa fedha 2026/2027.





No comments:
Post a Comment