HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 26, 2015

Chadema yawaonya viongozi wa dini mamluki

Na Bryceson Mathias, Mvomero


WANACHAMA wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Jimbo la Mvomero wamewaonya viongozi wa dini waliotia nia ya kugombea uongozi katika chama chao wasithubutu kuwa mamluki, kwa kuwa  watawashitaki kwa Mungu, na wakiendelea kwa shetani.

Akihojiwa na mwandishi kuhusu kuwepo kwa tuhuma za viongozi hao wanaodaiwa  kujipenyeza ndani ya Chadema kama mamluki, Katibu wa Chadema Mvomero, Ramadhani Mrisho, amewaonya viongozi hao kama wapo, kwa kuwa hakuna mharifu yeyote atakayepenya.

Hatua ya wanachama wa Chadema Mvomero kuwaonya viongozi hao, imefuatia kuwepo kwa fununu za watia nia hao kutumia fedha jimboni humo, ambapo walidai wanaunga mkono kauli ya Mwenyekiti wao, Freeman mbowe, ambaye hivi karibuni akiwa Mbeya aliwaonya wagombea wa Chadema kuwa  asiwepo atakayethubutu kutumia fedha kujipatia uongozi.

Mrisho alikiri kuwa anao viongozi wa dini zaidi ya wanne kutoka madhehebu mbalimbali waliotia nia ya kugombea uongozi tangu ngazi ya msingi hadi ubunge, huku akikiri na kusema kwa kutumia uwezo wao wameweza kukifikisha chama hadi  ngazi ya msingi.

“Hata mimi nimesikia minong’ono ya nje ya chama kuhusu baadhi ya viongozi hao kudaiwa wanatumia nguvu ya fedha kusaka uongozi huo. Lakini nataka nionye!  Kama atatokea mwenye nia ovu ya kukihujumu chama kwa njia hiyo, hatoki ng’o! Tutakula naye sahani moja!”

Aidha, alidai: “Nina imani kubwa na Kamati Kuu ya Chadema Taifa, kwenye kura ya maoni na uteuzi wa wagombea, kwamba itafanya kazi nzuri na ya haki, kutokana na jinsi ilivyo makini, maana, taarifa zote inazo kabla ya jogoo hajawika. Hivyo nina uhakika, kama mharifu yupo, hapenyi ng’o! Labda kamati iwe imeacha wajibu wake,” alisema Mrisho.

Mapema katika mchakato wa kuwania ubunge katika majimbo yanayoshikiliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), yanayowindwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wamejitokeza baadhi ya viongozi wa dini na watia nia mamluki, wanaodaiwa kutumika kuudhoofisha umoja huo kwa nafasi hizo ili kuwakwamisha Ukawa. 

No comments:

Post a Comment

Pages