HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 10, 2023

PSSSF YAPOKEA GAWIO LA SHILINGI BILIONI 14.82 KUTOKANA NA UWEKEZAJI BENKI YA CRDB


MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umepokea gawio la zaidi ya shilingi bilioni 14.82 baada ya kodi kutokana na uwekezaji wa hisa katika benki ya CRDB.

 

Hafla ya kukabidhi gawio kwa Serikali kuu na taasisi za umma kutokana na faida ambayo benki ilipata mnamo mwaka 2022 ilifanyika Ijumaa Juni 9, 2023 kwenye makao makuu ya CRDB jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.

Aidha Waziri Nchemba amefurahishwa na ongezeko la gawio la serikali na wanahisa wengine kuendelea kuongezeka kila mwaka.

“Nimefurahi kuona Taasisi na Mashirika ya Serikali, Halmashauri na Vyama vya Ushirika wamepokea gawio la shilingi bilioni 22.22 na hivyo kufanya jumla kuu ambayo Serikali imepokea gawio kutoka benki hiyo kuwa shilingi bilioni 46.88 ukilinganisha na gawio la mwaka jana ambalo serikali ilipokea la shilingi bilioni 36.1.

Akizungumzia gawio hilo la PSSSF kwaniaba ya Mkurugenzi Mkuu CPA. Hosea Kashimba, Mkurugenzi wa Fedha, Beatrice Musa-Lupi alisema gawio hilo ni ongezeko la zaidi ya asilimia 25% mwaka jana 2021 PSSSF ilipokea gawio la shilingi bilioni 11.85 baada ya kodi.

“Fedha hizi zinasaidia kuongeza thamani ya Mfuko kwa maana kwamba tutazirudisha kwenye uwekezaji lakini vile vile zinasaidia kuongeza ukwasi wa Mfuko kulipa mafao kwa wakati kama unavyofanya hivi sasa.” Alifafanua Mkurugenzi huyo wa fedha PSSSF.

“Uwekezaji huo unafanywa kwa kuzingatia sheria iliyoanzisha Mfuko ambayo inatoa wajibu wa kukusanya michango na wajibu wa kuwekeza ili kulinda thamani ya Michango ya Wanachama na kuleta uwajibikaji katika kulipa Mafao.” Alisisitiza Beatrice.

Alisema Mfuko unapofanya uwekezaji huangalia misingi ya uwekezaji kwa kuangalia mahala ambapo ni salama na kubainisha kuwa CRDB ni moja ya maeneo salama ambayo hisa za Mfuko ziko salama na zinaleta faida.

“Tunaamini CRDB itaendelea kufanya vizuri na faida itaendelea kupatikana na  gawio kuongezeka hivyo kuleta faida kwa wanahisa na wanachama wetu kwa ujumla.” Aliongeza Beatrice.

Naye Fortunatus Magambo, Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji PSSSF alisema Mfuko umewekeza asilimia 13.3 ya hisa zote za benki ya CRDB na anaamini gawio litazidi kuongezeka.

“Tunajivunia mafanikio haya na tunazidi kuwahimiza CRDB mwaka ujao tupokee gawio kubwa ziadi ya hili.” Alisema.

Kwa upande wake Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma PSSSF, Bw. James Mlowe alisema moja ya jukumu kubwa la Bodi ya Wadhamini na Menejimenti ya PSSSF ni kulinda maslahi ya wadau ambao ni wananchama na ndio maana wanahakikisha wanachagua wabia  sahihi wa kufanya biashara na uwekezaji.

“Kama tulivyoshuhudia tumepokea kiasi hicho ambacho si kidogo na niwaambie kuwa hii ni sehemu ndogo sana ya uwekezaji ambayo Mfuko umefanya kwani Mfuko umewekeza kwenye maeneo mbalimbali na hili ni hakikisho uwezo wa Mfuko kumudu majukumu yake ya kulipa Mafao.” Aliwahakikishia wanachama wa PSSSF.




No comments:

Post a Comment

Pages