HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 26, 2023

RBWB kujenga mabwawa mapya

 

 

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), akikata utepe wa uzinduzi wa Bwawa la Masaka lililopo wilayani Iringa.

Bwawa la Masaka lililopo kijiji cha Masaka mkoani Iringa likiwa limejaa maji kwa ajili ya uvuvi na kilimo.

 

Na Selemani Msuya

 

BODI ya Maji Bonde la Rufiji (RBWB) inatarajia kujenga mabwawa ya maji mapya matano katika mikoa wanayohudumia, ili kuhakikisha wananchi wanafanya shughuli za kilimo na uvuvi kwa njia enedelevu.

 

Aidha, RBWB imesema ujenzi wa mabwawa manne ya Masaka wilayani Iringa, Manda Chamwino, Mtamba Mpwawa na Itambolelo Mbarali upo katika hatua za mwisho.

 

Hayo yamesemwa na Ofisa Uhusiano wa Bodi hiyo Jacqueline Mmbiki wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii kwa njia ya simu kutoka Iringa.

 

Mmbiki alisema matarajio yao ni mwaka wa fedha 2023/24 ni kujenga mabwawa mapya matano katika maeneo ambayo yataanishwa, baada ya kukamilika hatua za usanifu.

 

“Tunarajia kujenga mabwawa mengine matano katika eneo letu la usimamizi katika mwaka wa fedha 2023/24, sisi tunataka kutekeleza maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa vitendo ambaye anataka vyanzo vya maji vitunzwe,” alisema.

 

Akifafanua kuhusu hatua zilizofikiwa kwenye ujenzi wa mabwawa manne ya Masaka, Manda, Mtamba na Itambolelo alisema kwa ujumla ujenzi umekamilika kwa asilimia 100 kwenye baadhi ya mabwawa.

 

Mmbiki alisema Bwawa la Manda limekamilika kwa asilimia 100 ambapo limeanza kufanya kazi na Bwawa la Masaka limeshawekewa firanga vya samaki.

 

“Bwawa la Mtamba limekamilika kwa asilimia zaidi ya 95, ila mvua zilikuwa chache, huku Itambolelo likiwa limejazwa maji, ila sehemu iliyobakia ni kwenye matoleo ya maji,” alisema.

 

Akizungumzia hali ya uharibifu wa vyanzo vya maji hasa katika eneo la Mbarali, alisema kwa sasa hali ni nzuri kutokana na kusimama shughuli za kilimo.

 

Alisema kwa sasa mifereji mingi imefungwa na muda wa vibali umesimama hivyo kusababisha mtiririko wa maji kuwa wa uhakika muda wote.

 

“Mbarali kwa sasa hakuna migogoro ya maji, kwani hakuna shughuli za kilimo. Lakini kwa ujumla vyanzo vya maji vipo salama kwa kuwa wakulima wapo kwenye mavuno, maji yanayotumika ni kwa matumizi ya nyumbani,” alisema.

 

Ofisa uhusiano huyo alisema pia kampeni ya upandaji miti ambayo ilizinduliwa na Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango imezidi kuboresha utunzaji wa vyanzo vya maji.

 

Aidha, Mmbiki alisisitiza kuwa katika kuvilinda vyanxzo vya maji wanatarajia kutumia walinzi maalumu kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania kuanzia mwaka wa fedha 2023/24.

 

Pia, alisema usimamizi wa vyanzo vya maji kwenye bonde hilo, umekuwa chanzo kikuu cha maji kujaa kwenye Bwawa la Kuzalisha Umeme la Julius Nyerere (JNHPP).


No comments:

Post a Comment

Pages